Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Vitisho dhidi ya wafanyakazi wa UM wahudumu wa misaada havikubaliki: UM

Vitisho dhidi ya wafanyakazi wa UM wahudumu wa misaada havikubaliki: UM

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati MINUSCA wametoa wito wakutokubaliana na vitisho vilinavyotolewa na muungano wa FPRC dhidi ya wafanyakazi wa MINUSCA, watendaji wa kibinadamu na raia. Ujumbe huo umeonya viongozi wa muungano huo kuwa watawajibika mmoja kwa mmoja kwa vitendo hivyo.  Katika taarifa yake iliyotolewa siku ya Jumamosi, MINUSCA imeonya kuwa mashambulizi yoyote kulenga raia, wafanya kazi wa misaada wa Umoja wa Mataifa ni uhalifu wa kivita ambao unaweza kufunguliwa mashitaka.

MINUSCA imesema kwamba hakuna kikundi cho chote kilicho na haki ya kuzuia au kuzorotesha upatikanaji wa misaada kwa jamii zilizo katika hatari na watendaji wa kibinadamu na hiyo basi imetoa wito hasa kwa muungano wa FPRC na makundi yote yenye silaha kujiepusha na matamko ya vitisho au kuzuia kazi ya wafanyakazi wa misaada .

Ujumbe huo umekataa madai ya FPRC kuwa wanachama wake watatu ambao walikamatwa na MINUSCA wakienda mjini Bambari walikuwa kwenye safari ya kutatua mzozo wa kutoelewana kati ya MINUSCA na wapiganaji.  Kwa mujibu wa ujumbe huo watu hao watatu walikuwa miongoni mwa watu arobaini ambao walisimamishwa kwa nguvu mnamo Februari 26. Watu hao na wanachama wengine wa FPRC walikiuka mpaka uliotengenezwa na MINUSCA wa kukaribia mji wa Bambari na silaha nzito za kuweza kusababisha hatari kwa mji na matokeo mabaya kwa raia.