Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ukosefu wa usalama wafurumusha watoa misaada 28 jimbo la Unity- OCHA

Ukosefu wa usalama wafurumusha watoa misaada 28 jimbo la Unity- OCHA

Nchini Sudan Kusini, wiki moja baada ya baadhi ya maeneo kutangazwa kukabiliwa na njaa, Umoja wa Mataifa umeomba pande kinzani kwenye mzozo nchini humo kuhakikisha usalama ili misaada ya kibinadamu iweze kuwafikia walengwa.

Ofisi ya umoja huo inayoratibu misaada ya kibinadamu, OCHA imesema njaa kwenye maeneo ya Leer ni sehemu ndogo tu ya maeneo yanayokabiliwa na njaa Sudan Kusini na sasa mapigano katika maeneo mbalimbali yanakwamisha usaidizi.

Mathalani OCHa imesema mapigano kwenye ukingo wa magharibi mwa mto Nile tangu mwezi Januari yamesababisha makumi ya maelfu ya raia kukimbia na sasa wako Kodok na Aburoc huku watoa huduma za misaada nao wakikumbwa na hofu.

Jens Laerke ni msemaji wa OCHA mjini Geneva, Uswisi.

(Sauti ya Jens)

“Watoa huduma za misaada 28 wamelazimika kuhama kutoka eneo la Mayendit jimbo la Unity, moja ya majimbo mawili yaliyoathirika zaidi kutokana na baa la njaa lililotangazwa.”

Wakati wa mapigano kwenye maeneo ya ukingo wa magharibi mwa mto Nile, watu wenye silaha na baada ya wananchi walivamia bohari zenye misaada na kupora.