Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Tutawalinda raia wa CAR gharama yoyote ile:Ladsous

Tutawalinda raia wa CAR gharama yoyote ile:Ladsous

Msaidizi wa Katibu Mkuu kuhusu operesheni za ulinzi wa amani Hervé Ladsous amewaambia wajumbe wa Baraza la Usalama kuwa leo Jumatano kuwa raia wa Jamhuri ya Afrika ya kati wamekabiliwa na mateso makubwa tangu mgogoro kuanza mwaka 2013 na hivyo basi ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini uko tayari kuwalinda raia hao dhidi ya makundi ya waasi hata kama ni kwa kuamua kutumia nguvu.

Akilihutubia baraza hilo Bwana Ladsous amesema kuwa japokuwa mji wa Bangui ni tulivu kwa wakati huu lakini bado kuna changamoto nyingi kwenye maeneo ya ndani ambapo hivi karibuni Februari 11, MINUSCA ililazimika  kutumia helikopta kwenye mashambulizi kuzuia kikundi cha wapiganaji wa waislamu zamani  wa Seleka kutofanya shambulio huko mjini Bambari.

Hivyo akatoa hakikisho.

(Sauti ya Ladsous)

MINUSCA itawalinda raia wakati wote kwa idhini ya azimio la UM na mkataba na serikali. Pia inaendelea na wajibu na utetezi wake kuwasiliana na makundi ya waasi kusitisha uhasama  mara moja na kuimarisha mawasiliano kwenye eneo hilo kaskazini-mashariki mwa Bambari ili kuzuia zaidi harakati zozote za waasi.

Bwana Ladsous ameongeza  kuwa mamlaka ya kitaifa imezindua kampeni mwezi jana Januari 30 kuwaajiri polisi 500 wa taifa ambao watapata mafunzo kutoka kwa Umoja wa Ulaya.

Hali ya kibinadamu inaendelea kuwa mbaya zaidi kutokana na ongezeko la vurugu katika mikoa, ikiwa pia na ukosefu wa fedha na uondokaji wa washirika wa misaada wa kutoa huduma za msingi nchini ambapo watu milioni 2.2 wana haja au uhaba wa chakula ikiwemo watu 100,000 wapya wanahitaji makazi.