Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Viongozi wa Afrika watoa ahadi ya kihistoria ya chanjo

Viongozi wa Afrika watoa ahadi ya kihistoria ya chanjo

Wakuu wa nchi za Muungano wa Afrika wametoa tamko la kihistoria la kuhakikisha kila mtu popote pale alipo barani humo anapata huduma za chanjo za msingi.Taarifa kamili na Amina Hassan.

(Taarifa ya Amina)

Tamko hilo lijulikanayo kama "Tamko la chanjo la Addis"  linatoa wito kwa nchi za Afrika kuongeza uwekezaji wa kisiasa na kiuchumi katika mipango yake ya chanjo na lina vipengele 10, ikiwa ni pamoja na kuongeza fedha katika mambo yanayohusu chanjo, kuimarisha minyororo ya ugavi na mifumo ya utoaji chanjo, na kufanya juhudi katika upatikanaji wa chanjo za msingi kwa maslahi ya afya na maendeleo.

Shirika la afya duniani, WHO linasema ingawa bara la Afrika limepiga hatua katika utoaji chanjo miaka 15 iliyopita, mafanikio hayo sasa yamezorota na kurudisha nyuma malengo ya chanjo ya kimataifa, na mmoja kati ya watoto watano barani humo hapati chanjo ya msingi, ikitolea mfano ugonjwa wa surua unaopora maisha ya watu 61,000 kila mwaka, jambo ambalo linaweza kuzuilika.

Wito huo umewezeshwa kwa ushirikiano wa WHO, Umoja wa Afrika, Shirika la chanjo la kimataifa Gavi na wadau wengine na limetiwa saini na Mawaziri wa Afya wa bara hilo .