Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IPU yampongeza Barrow, yasisitiza Jammeh aondoke

IPU yampongeza Barrow, yasisitiza Jammeh aondoke

Wakati kukiwa na hali ya sintofahamu nchini Gambia, muungano wa mabunge duniani IPU umempongeza Rais aliyeshinda uchaguzi na kuapishwa nchini Senegal Adama Barrow kwa ushindi wake.

Katika taarifa yake, IPU pamoja na pongezi hizo imemtaka Rais aliyekataa kuondoka madarakani Yahya Jammeh kuheshimu matokeo ya uchaguzi na kuhakikisha makabidhiano salama ya madaraka ili kuepuka vurugu na hatua za kijeshi.

‘‘Jaribio lolote la kusalia madarakani kwa njia zisizo halali ni kutoheshimu demokrasia na utawala wa sheria’’ amesema Martin Chungong, Katibu Mkuu wa IPU katika taarifa hiyo.

Amenukuliwa pia akisema kuwa ana matumaini kuwa Rais Barrow atarejea Gambia na kuanza kazi za kuwatumikia wananchi waliomchagua.