Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UN-HABITAT yakarabati makazi yaliyobomolewa Iraq

UN-HABITAT yakarabati makazi yaliyobomolewa Iraq

Shirika la Umoja wa mataifa la makazi duniani UN-Habitat limekabidhi nyumba 123 kwa wakazi waliorejea makwao kwenye kitongoji chaTameem , Ramadi mkoani Anbar nchini Iraq.

Taarifa ya UN-Habitat imesema kitongoji hicho ni eneo lililoharibiwa na kikundi cha kigaidi cha ISIL na operesheni za kijeshi mnamo desemba 2015, ambapo majengo yaliharibiwa na nyumba kuchomwa moto.

Mradi huo ujulikanao kama, “Kukuza miji katika maeneo mapya yaliyokombolewa nchini Iraq” umefadhiliwa kwa usaidizi pia na serikali ya Japan na ni moja ya miradi minne iliyozinduliwa na UN-Habitat kusaidia kuwarejesha watu waliokimbia makwao huko Ramadi.

Gavana wa Anbar, Sohaib Al-Rawi ameshukuru UN-Habitat kwa mradi huo na pia mashirika yote ya kimataifa akisema umesaidia kuleta utulivu na ahueni katika maeneo yaliyokombolewa kutoka ISIL.

 Mkuu wa UN-Habitat nchini Iraq Dkt Erfan Ali amesema shirika hilo litaendelea na mpango wake wa kukarabati nyumba zaidi ya 104 katika awamu ya pili na nyumba nyingine 200 mwaka 2017.