Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hali bado tete DRC, watu 20 waripotiwa kuuawa

Hali bado tete DRC, watu 20 waripotiwa kuuawa

Hali ya usalama kwenye mji mkuu wa Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo, DRC bado ni tete huku watu 20 wakiripotiwa kuwa wameuawa katika siku tatu zilizopita. Assumpta Massoi na ripoti kamili.

(Taarifa ya Assumpta)

Mjini Kinshasa, mazingira yameelezwa kuwa ni tofauti na kawaida, maduka yakiwa yamefungwa na watoto hawaendi shuleni wakati huu ambapo waandamanaji wanataka Rais Joseph Kabila aondoke madarakani kwa mujibu wa katiba.

Msemaji wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa huko DRC, MONUSCO Felix Basse ametoa takwimu hizo za vifo alipozungumza na Radio ya Umoja wa Mataifa ilhali serikali ikiripotiwa kusema idadi ya watu waliouawa wakati wa makabiliano kat ya polisi na waandamanaji ni Tisa.

(Sauti ya Felix)

“Ofisi ya pamoja ya haki za binadamu imepokea ripoti kadhaa kuwa watu 20 waliuawa wakiwemo wanawake watatu, na pia wengine 20 wamekamatwa na vikosi vya serikali.”

Bwana Basse amesema bado hawajaweza kutambua waliouawa au kukamatwa lakini ofisi hiyo inaendelea na uchunguzi na mawasiliano ili kuthibitisha ripoti hizo.