Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

WHO yanusuru waliozingirwa Allepo.

WHO yanusuru waliozingirwa Allepo.

Shirika la afya yulimwenguni WHO kwa kushirikiana na wadau wanatoa misaada ya uokozi wa maisha na huduma za kiafya kwa maelfu ya watu wanaokimbilia maeneo salama mjini Aleppo nchini Syria, kufuatia machafuko yanayoendelea.

Taarifa ya WHO inasema zaidi ya watu 250,000 wamezingirwa mjini humo, wakikabiliwa na uhaba wa chakula, dawa, maji na mafuta. Hospitali zote mjini Allepo zimefungwa au hufanya kazi mara chache hatua inayozidisha madhila kwa maelfu wanaohitaji msaada wa kiafya.

WHO inasema kuwa kadri hali ya kibinadamu inavyozidi kuzorota, watu zaidi ya 31,500 ni wakimbizi wa ndani hususani Magharibi mwa mji ambako raia wanakabiliwa na machafuko yanayoendelea na hospitali zimezidiwa uwezo kutokana na idadi kubwa ya majeruhi.

Shirika hilo la afya ulimwenguni hata hivyo limesema kwa kushirikiana na wadau wa afya lina misaada ya kutosha kwa ajili ya Magharibi mwa Aleppo, kusaidia takribani watu 80,000 kupitia vituo vya afya, timu zinazozunguka na huduma ya uokozi wa maisha kupitia hospitali.