Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Muswada wa NGOs Misri watishia uwepo wa mashirika hayo- Mtaalamu

Muswada wa NGOs Misri watishia uwepo wa mashirika hayo- Mtaalamu

Mtaalamu maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu uhuru wa kujieleza, Maina Kiai ameelezea wasiwasi wake juu ya mustakhbali wa mashirika ya kiraia, NGOs nchini Misri kutokana na muswada unaotarajiwa kupitishwa. Taarifa kamili na Rosemary Musumba.

(Taarifa ya Rosemary)

Katika taarifa yake, Maina amesema rasimu hiyo ya sheria inaweka udhibiti mkubwa wa mashirika ya kiraia na iwapo utapitishwa utasambaratisha mwelekeo wao na kusalia vibaraka wa serikali.

Mathalani ametaja moja ya kipengele ambacho kinapatia serikali mamlaka ya kuchagua nani aunde kikundi na kwa madhumuni yapi.

Amesema serikali haikuwa na mashauriano yoyote na mashirika hayo kuhusu muswada huo wa sheria ambao tayari bunge la Misri liliupitisha tarehe 15 mwezi huu na kuwasilisha mbele ya Baraza la kitaifa kwa ajili ya mapitio kabla ya kurejeshwa bungeni kwa kura ya mwisho katika tarehe ambayo bado haifahamiki.

Kwa mantiki hiyo Bwana Kiai ameomba mamlaka za Misri zisitishe mara moja mchakao wa kuridhia muswada huo.