Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mikunde ndio suluhu kwa lishe na rutuba ya ardhi- FAO

Mikunde ndio suluhu kwa lishe na rutuba ya ardhi- FAO

Mwaka wa mazao ya mikunde ukielekea ukingoni, shirika la chakula na kilimo duniani, FAO limesema uelewa wa walaji kuhusu faida za kiafya na lishe zitokanazo na ulaji wa mlo utokanao na mazao hayo bado umesalia mdogo.

Naibu Mkurugenzi Mkuu wa FAO, Maria Helena Semedo amesema hayo kwenye mjadala wa kimataifa wa mwaka wa mikunde huko Roma, Italia, mjadala unaofikia ukingoni leo.

Ametaja kunde, choroko, njugumawe na nyinginezo akisema bado hazijapatiwa umuhimu wa kutosha licha ya kuwa na kiwango kikubwa cha protini na pia kuboresha udongo na ustawi wa mazao mengine mashambani.

Bi. Semedo amesema mikunde isithaminiwe tu kinadharia bali pia kivitendo kupitia sera madhubuti inazostahili.

Katika mkutano huo, Malawi imesema kilimo cha pamoja cha mahindi na mikunde kimeongeza kipato na uhakika wa chakula, ilhali nchini Zambia, wanawake wanalima nusu ya mikunde inayosambazwa kwenye mlo shuleni.