Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Marekani isitishe mara moja kunyongwa kwa Kevin Cooper

Marekani isitishe mara moja kunyongwa kwa Kevin Cooper

Kundi la waatalamu huru wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa limeisihi Marekani isitishe mara moja hukumu ya kunyongwa hadi kufa dhidi ya Kevin Cooper.

Katika taarifa yao iliyotolewa leo, watetezi hao wa haki wametoa rai hiyo kwa gavana wa jimbo la California wakisema kuwa mchakato mzima hadi Cooper anahukumiwa adhabu hiyo kwa madai ya kuua wanandoa na mtoto wao, haukuwa wa haki.

Wamesema licha ya ushahidi ya kwamba mauaji hayo yalitekelezwa na watu kadhaa, polisi walisisitiza Cooper ndio mwenye hatia.

Cooper ambaye ni mmarekani mweusi, alikamatwa mwezi Julai mwaka 1983 nje kidogo ya jiji la Los Angeles kwa tuhuma hizo, huku ikielezwa kuwa mchakato mzima wa mahakama ukighibikwa na ushahidi wa uongo na uliorubuniwa.

Watetezi hao wa haki wamesema iwapo hukumu hiyo itatekelezwa, itakuwa ni kinyume na haki za binadamu.