Mitaala ya elimu Uganda kujumuisha udhibiti athari za majanga
Kufuatia ongezeko la majanga ya asili yanaosababishwa na mabadiliko ya tabianchi nchini Uganda, serilkali imejumuisha mafunzo ya upunguzaji wa athari za majanga katika mitaala ya shule za msingi. John Kibego na taarifa kamili
(Taarifa ya John Kibego)
Mkurugenzi wa Kituo cha Taifa cha kuunda Mitaala, Grace Baguma amesema, hatua hii inalenga kupata kizazi ambacho kinafahamu jinsi ya kukabiliana na majanga, kwani ni jambo jipya ambalo jamii inapaswa kuelewa.
Amesema, wanafunzi walio kati ya umri wa miaka 4 hadi 8 watafundishwa kwa kutumia michoro, huku walio kati ya miaka nane hadi kumi na mitatu watafundishwa kuandika taarifa kuhusu majanga miongoni mwa njia nyingine za kuimarisha uelewa.
Hatua hii itatimiza ndoto ya 2015 ya Ofisi ya Waziri Mkuu wa Uganda na Kitengo cha Usimamizi wa Majanga cha Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa iliotaka mafunzo ya upunguzaji wa athari za majanga yajumwishwe katika mitaala ya shule za msingi.
Watu zaidi ya milioni 1.8 nchini Uganda wamekimbia makaazi yao kutokana na mafuriko, maporomnoko ya ardhi na ukame tangu 1998.