Usaidizi kwa ajili ya wakimbizi upatiwe udharura- Grandi
Kamishna Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR Filippo Grandi amesema kadri janga la wakimbizi linavyozidi kupanuka, inakuwa vigumu kwa nchi moja pekee inayowapokea kuweza kuwapatia huduma za msingi na kwa uendelevu.
Bwana Grandi amesema hayo wakati akiwasilisha ripoti yake mbele ya kamati ya Tatu ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, kuhusu hali ya wakimbizi na wahamiaji duniani katika kipindi cha kuanzia tarehe Mosi Julai mwaka 2015 hadi Juni mwaka huu.
Amesema kwa kipindi hicho idadi ya wakimbizi wa ndani imeongezeka na kufikia Milioni 65 nukta Tatu, dharura mpya zitokanazo na mizozo zikizidi kung’oa watu makwao.

(Sauti ya Grandi)
“Uhaba wa fedha una madhara kwenye maeneo yote, lakini ina athari kubwa zaidi barani Afrika. Ukiwa na hali tete Somalia, Sudan Kusini na Jamhuri ya Afrika ya Kati, mahitaji yote ya kifedha yamechangiwa kwa chini ya asilimia 25. Hili ni pengo kubwa sana linalotia shaka na nadhani linapaswa ishughulikiwe kwa udharura.