Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wonder woman kuwakilisha wanawake na wasichana:UM

Wonder woman kuwakilisha wanawake na wasichana:UM

Mwanamke wa shoka na shupavu"Wonder woman" ametangazwa kuwa balozi wa Umoja wa Mataifa wa uwezeshaji wa wanawake na wasichana kuanzia leo Ijumaa. Rosemary Musumba na taarifa kamili

(TAARIFA YA ROSE)

Hatua hiyo inafuatia uamuzi wa Umoja wa Mataifa ambao unampa heshima kubwa na kumtangaza rasmi, mwanamke huyo ambaye ni kikaragosi maarufu katika ulimwengu kushika wadhifa huo.

Mwanamke huyo wa shoka anayetimiza miaka 75 mwaka huu katika uigizaji filamu za vikaragosi, jukumu lake jipya litakuwa zaidi ya kupambana na mashupavu wabaya , atabeba bendera ya Umoja wa Mataifa katika kuchagiza malengo ya maendeleo endelevu yaani SDG's hususani lengo nambari 5 ambalo ni kumuwezesha mwanamke na msichana kama kiungo muhimu cha kuleta amani, mafanikio na maendeleo endelevu duniani.

Pia atakuwa taswira ya kampeni hiyo katika mitandao ya kijamii . Watu mbalimbali watahudhuria hafla maalumu ya kutangazwa kwake kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa , wakiwemo Gal Gadot anaeigiza kama wonder womani siku hizi , lakini pia Lynda Carter, aliyecheza nafasi hiyo miaka ya 70.

Akizungumzia baada ya kikaragosi cha Wonder Woman kutangazwa kuwa balozi wa Umoja wa Mataifa, Diane Nelson, ambaye ni Rais wa kampuni ya DC Entertainment inayoshirikiana na Warner Bros kwenye kampeni hiyo amesema.

(Sauti ya Lynda)

“Nadhani jambo jema ambalo kampuni ya masuala ya burudani inaweza kuleta kwenye mashirika kama Umoja wa Mataifa ambayo  yanafanya kazi muhimu, ni kuleta mbinu ambazo zinaweza kuhamasisha juu ya masuala muhimu. Kwa hiyo kwa Wonder Woman una alama yenye maana fulani kwa watu wengi ulimwenguni kote.”

Akizungumza na wanahabari msemaji wa Umoja wa Mataifa Stephane Dujarric aliulizwa kuhusu hatua ya wafanyakazi 560 wa Umoja huo kuweka saini kwenye barua ya kupinga uteuzi wa Wonder Woman ambao amesema..

(Sauti ya Dujarric)

“Tunakaribisha kusikia maoni, maoni yanaweza kuwa yanakinzana na mradi. Bi Gallach amekutana na wawakilishi wa masuala ya jinsia na wengine na tutaendela kuwa na mjadala, nadhani kuna uwazi katika kukutana na watu wenye maoni tofauti.”