Hali ya walimu nchini Tanzania
Wiki hii tarehe Tano Oktoba, dunia imeadhimisha siku ya walimu duniani. Maslahi ya walimu, mafunzo na hadhi ya wanataaluma hawa vinajadiliwa dunia inapoadhimisha siku hii yenye kauli mbiu Thamini Walimu, Boresha Hali zao.
Umoja wa Mataifa kwa kutambua umuhimu wa taaluma hii katika mustakabali wa maendeleo, umepitisha lengo namba nne katika jaenda ya maendeleo ya 2030 mahususi kwa ajili ya elimu ambalo ni Elimu bora.
Katika kuadhimisha siku hii mashirika ya Umoja wa Mataifa lile la elimu,sayansi na utamaduni UNESCO, shirika la kuhudumia watoto UNICEF na lile la ajira ILO wakipigia upatu taaluma hiyo, yamesema walimu wana mchango mkubwa katika kunoa stadi za watoto ambao ni taifa na nguvukazi tegemezi katika siku zijazo.
Nchini Tanzania nako serikali inatekeleza mpango wa kukuza stadi za kusoma, kuandika na kuhesabu au KKK. Lakini je hali za walimu wanaotarajiwa kuwezesha mikakati hiyo ikoje? Tuelekee mkoa wa Kagera ulioko kwenye ncha ya kaskazini magharibi mwa Tanzania ambako Nicholas Ngaiza wa redio washirika KASIBANTE FM ameliangazia suala hilo.