Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Athari za kimbunga Matthew Haiti zinaweza kuwa janga kubwa:WMO

Athari za kimbunga Matthew Haiti zinaweza kuwa janga kubwa:WMO

Athari za kimbunga Matthew zinaweza kuwa janga kubwa kwa Haiti na jirani zake umesema Umoja wa mataifa Jumanne.

Likitoa onyo shirika la kimataifa la utabiri wa hali ya hewa (WMO), limearifu kuhusu upepo mkali unaokwenda kasi na kuzidi kilometa 230 kwa saa katika kitovu cha kimbunga hicho.

Kwa mujibu wa Clare Nullis msemaji wa shirika hilo mafuriko yaliyotabiriwa kuambatana na kimbunga hicho ndio suala linalotia hofu hasa Haiti, nchi ambayo bado inajikongoja baada ya tetemeko lililokatili zaidi ya watu 230,000 mwaka 2010.

(SAUTI YA CLAIRE NULLIS)

“Kimbunga kikubwa na kinakuja polepole, na hii inamaanisha kikienda polepole athari zake ni kubwa na hususani kwa Haiti zinauwezekano wa kuwa janga kubwa ni kauli ambayo inatamalaki.”

Shule hivi sasa zimefungwa kisiwani humo na zinatumika kama malazi ya muda, lakini hofu ni kwa watu 300,000 ambao huenda wakashindwa kuwasili katika makazi hayo kwa wakati kabla ya kimbunga hicho kuikumba Haiti, Jamhuri ya Dominika, Cuba na Bahamas.