Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Afrika ikifanikiwa nasi pia tutafanikiwa: Rais Hollande

Afrika ikifanikiwa nasi pia tutafanikiwa: Rais Hollande

"Natoa wito wa kuwepo kwa ajenda ya 2020 kwa ajili ya Afrika".Kauli hiyo imetolewa na Rais wa Ufaransa Françoise Hollande katika hotuba yake kwenye Kikao cha 71 cha Baraza Kuu. Amesema, Afrika ni bara lenye matumaini makubwa, lakini mandeleo yake yanarudishwa nyuma na mabadiliko ya tabianchi, uhamiaji, migogoro, vita na ugaidi.

Ameongeza kuwa ingawa kuna nuru Afrika katika siku za mbeleni, lakini pia kuna hatari kubwa ya ukosefu wa usalama, na walio hatarini zaidi ni wa Afrika wenyewe. Vile vile ameangazia suala la ukosefu wa umeme kupewa kipaumbele katika ajenda hiyo, akisema theluthi mbili ya watu wa bara hilo leo hii hawana umeme, jambo ambalo si haki, lakini kikubwa zaidi, ukosefu huo ni kikwazo dhidi ya ukuaji endelevu Afrika,na kusema

(HOLLANDE CUT)

"Changamoto tuliyonayo kwa hivyo ni kukidhi mahitaji ya asilimia 15 ya wakazi wa ulimwengu huu. Changamoto ni kuwezesha nchi za Afrika kufaidika na uwezo wao mkubwa. Changamoto ni kupunguza uhamiaji. Uhamiaji unayumbisha utulivu wa walikotoka na pia nchi wanakohamia."

Halikadhalika ametoa ahadi ya kuchangia asilimia 20 ya mchango wa bilioni 20 kwa Afrika, mchango ulioahidiwa na nchi 10 ifikapo mwaka 2020 kwa ajili ya nishati mbadala, na ametoa wito kwa nchi wanachama kuchangia mfuko huo, kwani maendeleo ya Afrika ni maendeleo ya ulimwengu mzima.

Akizungumzia suala la kusaini mkataba wa Paris kuhusu mabadiliko ya tabianchi amesema, Ufaransa imeridhia mkataba huo na hapo kesho atauwasilisha mbele ya Umoja wa Mataifa, akisihi nchi zingine zote zenye kuchangia asilimia 55 ya hewa chafuzi kuharakisha nyaraka zao.