Gabon rejesha intaneti na SMS na achia walioshikiliwa kisiasa- Ban
Vuguru zikiendelea kuripotiwa huko Gabon baada ya matokeo ya awali ya uchaguzi wa rais kumtangaza Ali Bongo kuwa mshindi, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ametaka serikali kurejesha njia za mawasiliano hasa intaneti na ujumbe mfupi, SMS.
Habari zinasema kuwa wananchi waliandamana kwenye mji mkuu Libreville, bada ya matokeo rasmi ya uchaguzi kumtangaza Rais Ali Bongo Ondimba kuwa mshindi kwa kura 5,500 zaidi ya mshindani wake. Moshi na moto vilionekana kutoka jengo la bunge usiku wa jumatano.
Katika ujumbe wake kwa njia ya radio kwa wananchi wa Gabon, Ban amesema..
“Nasihi mamlaka kuwaachia mara moja watu wanaoshikiliwa kwa misingi ya kisiasa na vile vile kurejesha njia za mawasiliano nchini humo.”
Ban amesema anatambua jinsi wananchi wa Gabon hasa vijana walivyokata tamaa wakitamania maisha bora na marekebisho ya kidemokrasia.
“Ni muhimu kwa wadau wote wa kisiasa na wanachi wa Gabon kujizuia na kumaliza tofauti zao kwa maslahi ya umoja wa kitaifa.”