Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Balozi mwema wa UNICEF azuru kambi yawakimbizi ya Za’atari Jordan:

Balozi mwema wa UNICEF azuru kambi yawakimbizi ya Za’atari Jordan:

Balozi mwema mpya wa shirika la Umoja wa mataifa la kuhudumia watoto UNICEF amezuru kambi ya wakimbizi ya Za’atari nchini Jordan.

Akiambatana na kinanda chake kikumbwa balozi huyo kwa ajili ya Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini Zade Dirani, amefanya ziara yake ya kwanza leo, kambini hapo na kwenye mji wa jirani wa Mafraq ili kutoa burudani ya muziki na ujumbe wa matumaini kwa watoto na vijana ikiwa ni pamoja na wale wote waliokimbia vita na ghasia nchini Syria.

Dirani amesema muziki una uwezo mkubwa wa kuvuka mipaka na kuwaleta watu wote pamoja katika nia ya ubinadamu.

Balozi huyo aliyeteuliwa wiki iliyopita amesem nia yake ni kuwaleta watoto na vijana pamoja kwa kutumia muziki leo na katika siku zijazo kama njia ya kuwahusisha lakini pia kama uponyaji kwa wale walioshuhudia madhila ambayo hakuna mtoto anayestahili kuyapitia.

Akiwa Za’atari, Dirani ametembelea kituo cha UNICEF cha “Makani” ambacho kinatoa msaada wa fursa ya kujifunza, ujuzi wa maisha na msaada wa kisaikolojia kwa watoto na vijana.