Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hatujatoa taarifa kupinga azimio la UM kuhusu kikosi cha kikanda-Rais Kiir

Hatujatoa taarifa kupinga azimio la UM kuhusu kikosi cha kikanda-Rais Kiir

Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini amezungumza kwenye uzinduzi wa bunge la kitaifa la mpito nchini humo na kutoa wito kwa wabunge kushirikiana kwa lengo la kujenga ushirikiano na stahmala.

Katika uzinduzi huo uliofanyika kwenye mji mkuu Juba, Rais Kiir amesema hawawezi kufikia kile ambacho wananchi wa Sudan Kusini wanatarajia iwapo hawatashirikiana na kuunga mkono uongozi mpya.

Hivyo ametoa wito kwa wabunge hao kustahimiliana na kushirikiana baina yao ili kufanikisha kile kinachotarajiwa kutoka kwao katika miezi ijayo.

Kuhusu azimio lililopitishwa Ijuma na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa la kuridhia kupelekwa Juba, kwa kikosi cha kikanda chenye wanajeshi 4,000, Rais Kiir amesema serikali yake haijatangaza kupinga uamuzi huo..

(Sauti ya Kiir)

“Tayari kuna watu ambao wanashutumu serikali ya kitaifa ya mpito, TGONU kwa kukataa na kupambana na Umoja wa Mataifa. Nataka nithibitishe siku hii muhimu kuwa huo siyo kauli sahihi ya msimamo wetu.

Halikadhalika amesema uchunguzi utaanzishwa kuhusu mazingira yaliyochochea kuibuka kwa ghasia huko Juba mwezi uliopita akisema kuwa tume ya uchunguzi itaundwa kufanya kazi hiyo.