Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kuharakisha unyongaji kutazidisha ukosefu wa haki Iraq: Zeid

Kuharakisha unyongaji kutazidisha ukosefu wa haki Iraq: Zeid

Kamishina mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa mataifa , Zeid Ra’ad Al Hussein Jumatatu ameelezea wasiwasi mkubwa kuhusu kamati iliyoundwa Iraq kwa lengo la kutoa mapendekezo ya kuharakisha utekelezaji wa hukumu za kifo nchini humo.

Kamati hiyo imepewa jukumu la kubaini taratibu au sheria zinazochelewesha utekelezaji wa hukumu za kifo zilizopitishwa na mahakama nchini humo. Zeid amesema wanawake , wanaume na watoto nchini Iraq wanaishi kwa hofu ya kupigwa mabomu, kuuawa, na ukatili mwingine hasa unaotekelezwa na kundi la ISIL.

Hivyo akasema katika mazingira hayo kuongeza vitendo vya unyongaji ni kuongeza madhila na ukosefu wa haki kwa watu hao.

Amesisitiza kuwa hofu yake zaidi ni kwamba, kutokana na mfumo dhoofu wa sheria, watu wengi wasio na hatia wataendelea kuhukumiwa na kunyongwa na huo ni ukkukwaji mkubwa wa haki.