Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watoto na barubaru bado waandamwa na VVU/Ukimwi- UNICEF

Watoto na barubaru bado waandamwa na VVU/Ukimwi- UNICEF

Shirika la Kuhudumia Watoto (UNICEF) limeonya kuwa licha ya hatua kubwa zilizopigwa kimataifa katika kupambana na janga la VVU na Ukimwi, bado kuna kazi kubwa ya kufanya katika kuwalinda watoto na vijana barubaru dhidi ya maambukizi, kuugua na kifo.

Onyo hilo limetolewa leo, wakati kongamano la 21 la kimataifa kuhusu Ukimwi likianza jijini Durban, Afrika Kusini wiki hii.

Tangu mwaka 2000, hatua madhubuti za kuzuia maambukizi kutoka kwa mama hadi kwa mtoto zimepunguza viwango vya maambukizi kwa asilimia 70 kote duniani, ikiwemo Kusini mwa jangwa la Sahara, ambako ndiko kwenye mzigo mkubwa zaidi wa maambukizi ya VVU na vifo.

Licha ya hatua hizo, UNICEF imesema barubaru wanafariki kutokana na Ukimwi kwa viwango vya kutia hofu, ikiongeza kwamba wasichana ndio hasa walio hatarini zaidi, wakichangia asilimia 65 ya maambukizi yote mapya duniani.