Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban ahuzunishwa na mapigano Sudan Kusini

Ban ahuzunishwa na mapigano Sudan Kusini

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon ameelezea kusikitishwa kwake kufuatia mapigano yanayoendelea kati ya jeshi la Sudan SPLA na vikundi vyenye silaha mjini Wau,  na maeneo jirani  nchini Sudan Kusini.

Taarifa ya msemaji wa Katibu Mkuu imemnukuu akisema kuwa amesikitishwa na taarifa za vifo kufuatia machafuko hayo.

Amevitaka vikosi kinzani kusitisha uhasama hima, kuruhusu ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini UNMISS kufika katika maeneo hayo na kushirikiana na wadau wa misaada ya kibinadamu ili kuwezesha ufikishwaji wa misaada.

Ban amezitaka pande hizo kukubali majadiliano ili kutatua mizozo yao ya kisiasa huku pia akipongeza UNMISS na timu ya misaada ya kibinadamu nchini humo kwa hatua za kulinda raia wanoakimbia mjini Wau.

UNMISS iko katika mchakato wa kutuma vikosi zaidi ili kukabiliana na dharura.