Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Jumuiya ya Ulaya chondechonde wathaminini wakimbizi,wahamiaji: Ban

Jumuiya ya Ulaya chondechonde wathaminini wakimbizi,wahamiaji: Ban

Akiwa ziarani nchini Ufaransa, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amesisisitiza kuwa uamuzi wa Uingereza kujitoa katika jumuiya ya Ulaya EU, haupasiwi kuwa mzigo kwa wakimbizi, wahamiaji na wasaka hifadhi barani humo.

Akizungumza na vyombo vya habari akiwa ameambatana na mwenyeji wake Rais Francois Hollande, Ban amesema anatarajia nchi za Ulaya zitaheshimu sheria za  kimataifa na kuonyesha ubinadamu kwa makundi hayo yasiyo na hatia.

Akitolea mfano Katibu Mkuu amesema juma lililopita alitembelea kisiwa cha Lesbos nchini Ugiriki ambapo alikutana na kushuhudia madhila ya wakimbizi kutoka Syria, na Iraq.

Amesema wakimbizi hao ambao waliosafiri safari zisizo salama za muda mrefu ni wachovu na wanachotaka ni uslama na watoto wao, elimu na ajira ili waweze kushiriki katika maendeleo.