Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Usanii sio uhalifu, wasanii waliofungwa waachiliwe Iran:UM

Usanii sio uhalifu, wasanii waliofungwa waachiliwe Iran:UM

Mwakilishi maalumu wa Umoja wa mataifa kuhusu haki ya utamaduni Karima Bennoune, na yule wa uhuru wa kujieleza, David Kaye,leo wametoa wito kwa serikali ya Kiislam ya Iran, kuwaachilia wanamuziki Mehdi Rajabian na Yousef Emadi, pia mtayarishaji wa filamu Hossein Rajabian, ambao wamifungwa na kutozwa faini kubwa mapema mwezi huu.

Wasanii hawa watatu walihukumiwa kwa kutekeleza haki yao ya uhuru wa kujieleza na ubunifu suala ambalo ni matokeo ya vikwazo dhidi ya haki za watu nchini Iran kuweza kupata na kufurahia Sanaa amesema Bi Bennoune.

Ameongeza kuwa kujieleza kisanii sio uhalifu. Wataalamu wa haki za binadamu wamewasiliana na serikali ya Iran kuhusu kesi hizo mapema mwaka huu ikiwa ni pamoja na matumizi ya mateso dhidi ya mwanamuziki Rajabian,ambaye pia ni mwanzilishi wa kampuni ya Barg Music,mbadala wa usambazaji wa muziki nchini Iran.