Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IOM yatiwa wasiwasi na idadi ya vifo vya wahamiaji Afrika

IOM yatiwa wasiwasi na idadi ya vifo vya wahamiaji Afrika

Shirika la kimataifa la Uhamiaji IOM limesikitishwa na ripoti za kubainika kwa maiti ya wahamiaji 34 kwenye mpaka wa Niger na Algeria wiki hii.

Yaripotiwa kuwa maiti hao ni ya wahamiaji waliotelekezwa na mtu ambaye alikuwa anawasindikiza.Kwa mujibu wa IOM, idadi ya wahamiaji waliofariki dunia au kutoweka barani Afrika mwaka huu sasa imefikia 471.

Kwenye taarifa iliyotolewa leo, IOM imeeleza kwamba watu angalau 250 wamefariki dunia kwenye jangwa la Sahara pekee, kutokana na joto kali, njaa na kiu. Halikadhalika, kesi za mauaji katili zimeongezeka Afrika Kaskazini, IOM imeongeza, pamoja na visa vya utesaji, vingi vikiwa haviripotiwi.