Watu zaidi ya milioni 1 Msumbiji wahitaji msaada kutokana na athari za El Niño-OCHA
Watu takribani milioni 1.5 wanahitaji msaada nchini Msumbiji kutokana na ukame mkubwa uliosababishwa na El Niño. Hayo ni kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuratibu masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura OCHA.
Shirika hilo linasema nusu ya watu walioathirika wametathiminiwa kuwa katika matatizo makubwa ya chakula na maisha magumu hasa vijijini, huku watoto wapatao 95,000 wakikabiliwa na utapiamlo au kukaribia kupata hali hiyo inayotishia maisha yao.
OCHA inasema ukosefu wa mvua mwaka jana umeathiri mavuno ya wakulima karibu 460,000 wanaotegemea mazao kama mahindi na mihogo kwa chakula. Jens Laerke ni msemaji wa OCHA
(SAUTI YA JENS LAERKE)
“Timu ya masuala ya kibinadamu nchini humo kwa ushirikiano na serikali wamezindua mkakati wa miezi 12 wa kutoa chakula, lishe, maji na huduma za kujisafi pamoja na ulinzi kwa watu milioni 1.5. Mpango huo unahitaji dola milioni 203 lakini umepokea ufadhili wa dola milioni 13 tu.”