Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kambi ya MINUSMA yashambuliwa Mali

Kambi ya MINUSMA yashambuliwa Mali

Mlinda amani mmoja ameuawa jumanne usiku nchini Mali, kambi ya Ujumbe wa Umoja wa MAtaifa nchini humo MINUSMA iliposhambuliwa na makombora. Flora Nducha na taarifa kamili

(TAARIFA YA FLORA)

Kwenye taarifa iliyotolewa leo, MINUSMA imeeleza kwamba kambi yake iliyoko mjini Gao, kaskazini mwa nchi, ilipigwa na makombora na roketi jumanne usiku.

Walinda amani watatu wamejeruhiwa pia kwenye shambulio hilo pamoja na zaidi ya wafanyakazi wengine 10 wa MINUSMA.

Shambulio hilo limefuatiwa na shambulio lingine dhidi ya ofisi ya mtoa huduma wa UNMAS, Shirika la Umoja wa Mataifa la Kupambana na mabomu yaliyotegwa ardhini, ambapo watu watatu wameuawa.

Mkuu wa MINUSMA Mahamat Saleh Annadif ameeleza kushtushwa sana na mashambulizi hayo akiisihi serikali ya Mali kuhakikisha watekelezaji wanapelekwa mbele ya sheria. Ametuma pia salamu zake za rambirambi kwa familia za wahanga.