Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IOM burundi kusaidia wahamiaji waliorejeshwa Rwanda

IOM burundi kusaidia wahamiaji waliorejeshwa Rwanda

Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) nchini Burundi, limesema linawapatia msaada raia wa Burundi waliofukuzwa kutoka Rwanda siku chache zilizopita kwa kutokua na vibali vya kuwa nchini Rwanda. Taarifa zaidi na Priscilla Lecomte.

(Taarifa ya Priscilla)

Kwa mujibu wa IOM Burundi, mashirika ya kibinadamu nchini humo yameamua kutekeleza mpango wa pamoja wa kutimiza mahitaji ya dharura ya wahamiaji hao ambao wameripotiwa kurejeshwa Burundi bila kuruhusiwa kuchukua mali zao, wengine wakilazimishwa kuacha mke na watoto.

Miongoni mwa misaada itakayotolewa ni chakula, vifaa mbali mbali, huku juhudi za kukutanisha upya familia na kuwapatia mali zao zikifanywa pia

Wahamiaji hao wapatao 1,500 wameripotiwa kufukuzwa kutoka Rwanda, wakiwa hawana vibali vya makazi, ingawa baadhi yao walikuwa wameishi Rwanda kwa miaka mingi.

IOM imeongeza kwamba ripoti zilizokusanywa zinaonyesha kwamba wahamiaji hao wameambiwa ama wajisajili kwenye kambi za wakimbizi Rwanda, ama warejeshwe Burundi, na kwa mujibu wa IOM shughuli hizo zimefanywa bila ukatili.