Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Umoja wa Mataifa kuongeza mamlaka za UNISFA Abyei

Umoja wa Mataifa kuongeza mamlaka za UNISFA Abyei

Baraza la Usalama leo limepitisha kwa kauli moja azimio la kuongeza muda wa mamlaka za Vikosi vya Usalama vya muda vya Umoja wa Mataifa kwenye jimbo la Abyei, UNISFA. Taarifa zaidi na Priscilla Lecomte.

(Taarifa ya Priscilla)

Mamlaka za UNISFA zimeongezwa muda hadi Novemba, 15, mwaka 2016, kwa lengo la kuhakikisha eneo la Abyei lililo mpakani mwa Sudan na Sudan Kusini linakuwa na utulivu na haliingiliwi na vikosi vya usalama vya Sudan wala Sudan Kusini. Azimio la leo linasisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Sudan na Sudan Kusini katika kukuza utulivu na kuunda taasisi za muda za eneo hilo, kwani hadi sasa hakuna mamlaka yoyote inayotawala Abyei.

Wanachama wa Umoja wa Mataifa wameiomba UNISFA pia kuendelea kukuza maridhiano na mazungumzo ya jamii kati ya makabila ya Misseriya na Ngok Dinka yanayoishi Abyei na kufuatilia hali ya haki za binadamu. Watu wapatao 140,000 wanategemea misaada ya kibinadamu kwenye eneo hilo, wakikumbwa na ukame na mivutano ya kikabila.