Mfumo wa sheria Ushelisheli wapongezwa kwa kukabili uharamia:Ban
Mfumo wa sheria nchini Ushelisheli umepongezwa kwa kazi nzuri ya kukabiliana na uharamia katika mwambao wa bahari ya Hindi lakini pia uhalifu mwingine.
Akizungumza kwenye mahakama ya haki (Kasri la haki) alipokutana na mwanasheria mkuu kisiwani humo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amesema Ushelisheli ni kisiwa pekee ambacho kimefanikiwa kuwakamata na kuwahukumu maharamia wanaoendesha shughuli zao kwenye pwani ya bahari ya Hindi.
Ameongeza kuwa mfumo wa sheria wa Ushelisheli pia unashirikiana kwa karibu na ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kudhibiti madawa na uhalifu UNODC, katika vita dhidi ya mihadarati na usafirishaji haramu wa watu. Amesema yote haya ni katika kwenda sanjari na utekelezaji wa malengo ya maendeleo endelevu SDG’s na anashukuru kisiwa hicho kwa juhudi zake
(SAUTI YA BAN)
“Ninashukuru sana kwa uongozi wenu , ni nchi imara na najua kwamba ni kazi ngumu , lakini haya ndio tunayofanya kwa utu wa watu”
