Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hali ya kibinadamu Ukraine bado yatia shaka- Zerihouh

Hali ya kibinadamu Ukraine bado yatia shaka- Zerihouh

Mzozo Ukraine ukiingia mwaka wa tatu, baraza la usalama la Umoja wa Mataifa limeelezwa kuwa hali ya kibinadamu inazidi kuzorota na kutia wasiwasi mkubwa.

Akihutubia baraza hilo leo wakati wa kikao kuhusu hali nchini Ukraine, Naibu Msaidizi wa Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu masuala ya siasa Tayd-Brook Zerihoun, amesema zaidi ya watu Milioni Tatu wanahitaji misaada ya kibinadamu hususan wale walio karibu na maeneo yenye mapigano na ambako hakuna udhibiti wa serikali.

(Sauti ya Tayd-Brook)

“Kuendelea kusitishwa kwa ushirikiano kulikotangazwa na mamlaka huko Donetsk na Luhansk kwa karibu mashirika yote ya Umoja wa Mataifa na yasiyo ya kiserikali tangu Julai mwaka 2015 kunatia wasiwasi mkubwa. Urasimu usio na maana yoyote unawanyima maelfu ya watu kupata misaada muhimu inayohitajika haraka pamoja na huduma ya ulinzi.”

Hata hivyo Bwana Zerihoun amesema licha ya mashaka hayo, bado kumekuwepo na matumaini tangu kikao cha mwisho cha Baraza la Usalama kuhusu Ukraine mwezi Disemba mwaka jana akitolea mfano sitisho la mapigano wiki mbili za mwisho wa mwezi Disemba mwaka jana.