Ban na Kim wateua wanajopo la ngazi ya juu kuhusu maji
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon na Rais wa Benki ya Dunia, Jim Yong Kim, wametangaza leo uteuzi wa viongozi 10 wa nchi na serikali, pamoja na washauri wawili maalum, kuwa wanachama wa jopo la ngazi ya juu kuhusu maji.
Jopo hilo litakalosimamiwa na Rais Ameenah Gurib wa Mauritius, lilizinduliwa mnamo mwezi Januari wakati wa Kongamano la Uchumi Duniani huko Davos, likilenga kuchagiza hatua fanisi katika kuongeza kasi ya kutekeleza lengo la maendeleo endelevu namba 6, ambalo linaangazia udhibiti endelevu wa upatikanaji maji safi na huduma za kujisafi kwa wote.
Wanajopo hao watakahudumu kwa kipindi cha miaka miwili ni:
Bi. Ameenah Gurib, Rais wa Mauritius (Mwenyekiti)
Bw. Enrique Peña Nieto, Rais wa Mexico (Mwenyekiti Mwenza)
Bw. Malcolm Turnbull, Waziri Mkuu wa Australia
Bi. Sheikh Hasina, Waziri Mkuu wa Bangladesh
Bw. János Áder, Rais wa Hungary
Bw. Abdullah Ensour, Waziri Mkuu wa Jordan
Bw. Mark Rutte, Waziri Mkuu wa Uholanzi
Bw. Jacob Zuma, Rais wa Jamhuri ya Afrika Kusini
Bw. Macky Sall, Rais wa Senegal
Bw. Emomali Rahmon, Rais wa Tajikistan
Washauri maalum wawili ni
Dkt. Han Seung-soo, Waziri Mkuu wa zamani wa Jamhuri ya Korea (Kusini)
Bw. Manuel Pulgar-Vidal, Waziri wa Mazingira wa Peru
Katika taarifa iliyotangaza uteuzi huo, Katibu Mkuu Ban Ki-moon amesema, kuhakikisha upatikanaji wa maji safi na huduma za kujisafi kwa wote ni muhimu katika kupunguza umaskini na kutimiza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs), na kutoa wito kwa wadau wote kuunga mkono lengo la SDG namba 6 kisiasa, kifedha na kiteknolojia.