Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mchakato wa kumpata mrithi wa Ban waanza leo

Mchakato wa kumpata mrithi wa Ban waanza leo

Mchakato wa kumpata Katibu Mkuu mpya wa Umoja wa Mataifa atakayechukua nafasi baada ya Ban Ki-moon kuhitimisha muhula wake mwishoni mwa mwaka huu umeanza hii leo jijini New York, Marekani. Grace Kaneiya na Ripoti kamili.

(Taarifa ya Grace)

Mchakato unahusisha mazungumzo yasiyo rasmi na wagombea wote wanane, wakiulizwa maswali kutoka mashirika ya kiraia. Mchakato utaendelea hadi tarehe 14 mwezi huu ambapo leo wanaohojiwa ni watatu ambao ni Dkt. Igor Luksic kutoka Montenegro, Irina Bokova kutoka Bulgaria na Antonio Guterres kutoka Ureno.

Akifungua mchakato huo Rais wa Baraza Kuu la Umoja Mataifa Mogens Lykketoft amesema hii ni mara ya kwanza katika historia ya Umoja wa Mataifa kwa mchakato wa uteuzi na uchaguzi kuongozwa kwa misingi ya uwazi na ushirikishi akisema

(Sauti ya Lykketoft)

“Mchakato huu unatoa fursa kwa Baraza kujithibitisha, kuweka viwango vipya vya uwazi na ushirikishi katika michakato ya Umoja wa Mataifa na muhimu zaidi kusaidia kupata mgombea bora atakayekuwa Katibu Mkuu wetu ajaye.”

image
Igor Lukšić mmoja wa wagombea wa nafasi ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa. (Picha:UN/Rick Bajornas)
Na ndipo wagombea watatu kati ya wanane wakaanza kujieleza na wa kwanza alikuwa Dkt. Igor Luksic Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa mambo ya kigeni wa Montenegro. Katika hotuba yake tangulizi amesema changamoto kubwa zinazokabili dunia sasa zahitaji kiongozi anayweza kufanya chombo hicho kiendelee kuwa na maana na kifanye kazi kwa bidi.
image
Irina Bokova, mmoja wa wagombea wa nafasi ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa. (picha:UN/Manuel Elias)
Irina Bokova kutoka Bulgaria, ni Mkurugenzi Mkuu wa shirika la elimu, sayansi na utamaduni la Umoja wa Mataifa, UNESCO naye anawania nafasi ya Ukatibu Mkuu. Moja ya mambo aliyogusia ni ushiriki wa kanda mbali mbali duniani katika kufanikisha ajenda ya maendeleo endelevu, SDGs.
image
António Guterres, mmoja wa wagombea wa nafasi ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa. (picha:UN/Manuel Elias)
Na pazia la mazungumzo na kuhojiwa kwa siku ya Jumanne lilifungwa na Kamishna Mkuu mstaafu wa shirika la wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR Antonio Guterres kutoka Ureno. Yeye alijikita katika suala la umuhimu wa kusaka suluhu la mizozo ili kuondokana na majanga ya kibinadamu yanayokumba dunia hivi sasa.

Mazungumzo hayo yanayoratibiwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa yataendelea kesho.