Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ujenzi wa maktaba kubwa zaidi kwa wakimbizi wa Palestina waendelea- UNRWA

Ujenzi wa maktaba kubwa zaidi kwa wakimbizi wa Palestina waendelea- UNRWA

Kazi ya ujenzi wa maktaba kwa ajili ya shule ya msingi ya Rafah huko Gaza Kusini, iliyoanza mwezi Disemba mwaka jana, inaendelea na inatarajiwa kukamilika mwezi Septemba mwaka huu.

Shirika la Umoja wa Mataifa la misaada kwa wakimbizi wa kipalestina, UNRWA lilikabidhi ujenzi huo kwa kampuni binafsi na hadi sasa umefikia asilimai 30 na kwamba itakapokamilika itakuwa ni maktaba kubwa zaidi kwenye kambi ya wakimbizi ya Rafah.

UNRWA imesema lengo ni kuongeza kiwango cha kujua kusoma na kuandika kwenye jamii hiyo pamoja na kuhamasisha watoto kusoma na kutafakuri sanjari na kusaidia mtaala wa shule.

Maktaba hiyo itatumiwa siyo tu na wanafunzi na walimu wa shule hiyo bali pia itakuwa wazi kwa umma wakiwemo wakimbizi na ujenzi wake unafuatia usaidizi kutoka shirika la misaada la kifalme la Bahrain.