Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uchukuaji sheria mkononi Malawi watia hofu UM

Uchukuaji sheria mkononi Malawi watia hofu UM

Ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa inatiwa wasiwasi mkubwa kutokana na ongezeko la umma kuchukua sheria mkononi nchini Malawi na kuua watu kwa tuhuma mbali mbali ikiwemo ushirikina.

Msemaji wa ofisi hiyo Cécile Pouilly amesema katika kipindi cha miezi miwili iliyopita kumekuwepo na matukio yapatayo Tisa yakisababisha watu 16 kuuawa maeneo mbali mbali nchini humo.

Miongoni mwa matukio hayo ni watu kuvamia kituo polisi na kumchukua mtuhumiwa wa mauaji na hatimaye kumuua pamoja na wazee wanne kuuawa kwa tuhuma za kumtumia radi mwanamke mmoja kwa uchawi na hatimaye kumuua.

Bi. Poilly anasema wanakaribisha hatua ya Rais Arthur Mutharika wa Malawi la kulaani vitendo hivyo na kwamba..

“Tunatoa wito kwa mamlaka za Malawi kuchukua hatua haraka kubaini na kuwashtaki wote waliohusika na uchukuaji sheria mkononi pamoja na kuwalipa fidia wahanga. Serikali pia ichunguze vyanzo vya mashambulizi hayo na kuelimisha umma kuripoti uhalifu polisi badala ya kuchukua sheria mkononi.”