Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kisa kipya cha Ebola chathibitishwa Liberia:WHO

Kisa kipya cha Ebola chathibitishwa Liberia:WHO

Shirika la afya ulimwenguni WHO limethibitisha kisa kipya cha homa kali ya Ebola nchini Liberia, kufuatia kifo cha mwanamke mwenye umri wa miaka 30 aliyefariki dunia jana mchana wakati akihamishiwa hosipitali mjini Monrovia.

WHO katika taarifa yake imesema kuwa kwa kushirikiana na wizara ya afya ya Liberia na wadau wengine wa afya, walitumatimu katiak jamii alipokuwa akiishi mgonjwa huyo na kliniki alipokuwa anatibiwa ili kuanzisha uchunguzi ukiwemo pia kwa watu ambao wamekuwa karibu naye.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mamalaka za afya nchini humo zimekuwa na kikao cha dharura na wadau muhimu asubuhi ya leo, kuratibu hatua za dharura kufuatia kisa hicho katika taifa ambalo lilitangazwa kuitokomeza Ebola.

Mapema wiki hii kamati ya kimtaifa ya miongozo ya dharura za kiafya na WHO zilitangaza kuwa ugonjwa wa Ebola sio dharura ya kimataifa tena katika ukanda wa Afrika Magharibi.