Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hatua kidogo sana zimepigwa kukabiliana na ubaguzi wa rangi na chuki dhidi ya wageni:UM

Hatua kidogo sana zimepigwa kukabiliana na ubaguzi wa rangi na chuki dhidi ya wageni:UM

Katika kuelekea siku ya kimataifa ya kupinga ubaguzi wa rangi hapo Jumatatu Machi 21, dunia inashuhudia ongezeko la kutisha la chuki na hotuba za chuki dhidi ya wageni , wamesema wataalamu watatu wa Umoja wa Mataifa kuhusu ubaguzi na ubaguzi wa rangi.

Kwa mujibu wa wataalamu hao Mutuma Rutereere mwakilishi maalumu kuhusu mifumo ya kisasa ya ubaguzi wa rangi, mwakilishi maalumu na mwenyekiti wa kundi maalumu la waatalamu kuhusu watu wenye asili ya Afrika, Mireille Fanon Mendes-France na mwenyekiti wa kamati ya utokomezaji wa ubaguzi wa rangi Jose Francisco Cali Tzay, juhudi zaidi zinahitajika kufanywa na serikali kote duniani kulinda makundi yaliyo katika hatari na kuwaadhibu wanaotekeleza ukatili huo.

Wameongeza kuwa miaka 15 baada ya mkutano wa Durban hatua ndogo sana imepigwa kukabiliana na ubaguzi wa rangi, chuki dhidi ya Uafrika, ubaguzi kwa misingi ya rangi, chuki dhidi ya wageni na masuala mengine yanayoshabihiyana na hayo na badala yake kunashuhudiwa ongezeko kubwa la chuki, na hotuba za chuki dhidi ya wageni duniani kote.

image
Wameongeza kuwa ukwepaji sheria umekuwa kama ada kwa uhalifu uliopindukia na hii ni hali ya kutia hofu.
Wameonya kwamba viongozi wa kisiasa, watu mashuhuri katika jamii na hata vyombo vya habari vinawanyanyapaa na kuwadhihaki wahamiaji, wakimbizi, waomba hifadhi na wageni kwa ujumla pamoja na walio wachache. Wameelezea hofu yao juu ya wito wa karibuni wa wanasiasa na maafisa wa serikali wa kutaka maelfu ya wageni kukamatwa na kurudishwa makwao kwa nguvu wakisema tabia hii inachagiza vitendo vya ghasia dhidi ya wale walio katika hatari. Wametoa wito kwa serikali kuanzisha mipango maalumu ya hatua za kupinga ubaguzi wa rangi pamoja na vyombo vya kutoa msaada kwa waathirika.