Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uharibifu wa urithi wa kitamaduni ni ukiukwaji wa haki za binadamu- mtaalam wa UM

Uharibifu wa urithi wa kitamaduni ni ukiukwaji wa haki za binadamu- mtaalam wa UM

Mtaalam maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za kitamaduni, Karima Bennoune, amesema leo kuwa ni vigumu kuutenganisha urithi wa kitamaduni wa watu na haki zao, akiongeza kuwa uharibifu wa urithi huo ni ukiukwaji wa haki za binadamu.

Bi Bennoune amesema hayo wakati Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) ikianza kusikiliza thibitisho la mashtaka yanayohusu uharibifu wa maeneo ya urithi wa kitamaduni, Timbuktu, Mali.

Mtaalam huyo ametaka uharibifu wa urithi wa kitamaduni unaofanywa na serikali na vikundi visivyo vya kiserikali ushughulikiwe hima na jamii ya kimataifa, akisema ieleweke dhahiri kuwa kila urithi wa kitamaduni unaposhambuliwa, basi haki za watu za msingi zinashambuliwa.

Amekaribisha uamuzi wa Ofisi ya Mwendesha Mashtaka Mkuu wa ICC kuushtaki uharibifu wa urithi wa kitamaduni na maeneo ya dini na majengo ya kihistoria kama uhalifu wa kivita.