Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Jamii ya kimataifa ni lazima itimize wajibu wa kulinda raia- Eliasson

Jamii ya kimataifa ni lazima itimize wajibu wa kulinda raia- Eliasson

Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Jan Eliasson, ametoa wito kwa jamii ya kimataifa ithibitishe wajibu wake wa kulinda raia, kama ilivyo weka ahadi katika mkutano wa mwaka 2005.

Bwana Eliasson amesema hayo akilihutubia jopo la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, ambalo limekutana kujadili kuhusu utekelezaji wa dhamira ya wajibu wa kulinda, miaka kumi tangu dhana hiyo ilipoanzishwa kwenye mkutano wa kimataifa.

Akihoji hatua zilizopigwa miaka kumi tangu ahadi hiyo kuwekwa, Bwana Eliasson ameuliza

image
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Jan Eliasson.(Picha:UM/Manuel Elias)
“Je, tumesonga kutoka ahadi na kuanza kutekeleza? Hapana, naweza kusema hatujapiga hatua sana. Tukitizama duniani, tunaona hali ambapo raia wanapitia mateso makubwa. Mengine huenda yakawa ni mauaji ya kimbari, uhalifu wa kivita, uangamizaji wa kikabila na uhalifu dhidi ya ubinadamu.”

Amesema ahadi iliyozalisha dhana ya wajibu wa kulinda haikuwa kukariri maadili ya ubinadamu kwa maneno tu, bali ilikuwa wito wa kuchukua hatua

“Ni lazima tufanye kazi pamoja ili kuhakikisha kuna ulinzi wa watu kutokana na mauaji ya kimbari, uangamizaji wa kikabila, uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya ubinadamu. Huu ni wajibu wetu kwa ubinadamu, na kwa watu tunaohudumia katika moyo wa Katiba ya Umoja wa Mataifa.”

Akizungumza wakati wa mjadala huo, Mshauri maalum wa Katibu Mkuu kuhusu kuzuia mauaji ya kimbari, Adama Dieng, ambaye ameongoza mjadala huo, amesema nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa zina wajibu wa kuchagiza na kuanza kutekeleza kanuni ya wajibu wa kulinda

image
Mshauri maalum wa Katibu Mkuu kuhusu kuzuia mauaji ya kimbari, Adama Dieng.(Picha:UM/Rick Bajornas)
Mwaka 2005, viongozi wa dunia walikuja hapa New York na kuafikia kanuni hii. Hii ni kwa sababu, viongozi hawa na watu duniani, walishtushwa na majanga yaliyotokea katika nusu ya pili ya karne ya 20. Na nazungumzia kilichotokea Rwanda, 1994, kwa mauaji ya kimbari ya Watutsi na Srebrenica. Baada ya 1945 dunia ilikuwa imesema, haitatokea kamwe tena, lakini nasikitika kuwa tulishuhudia tena utendaji wa mauaji haya ya kihalifu, na hii haikubaliki”