Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mabadiliko ya tabianchi na El Niño vilichangia majanga ya 2015- UM

Mabadiliko ya tabianchi na El Niño vilichangia majanga ya 2015- UM

Mwaka wa 2015, ambao ulikuwa wenye joto kali zaidi duniani kuwahi kurekodiwa, umethibitisha kwamba majanga yanayotokana na hali ya hewa na tabianchi sasa yametawala mienendo ya majanga ya kiasili, kwa mujibu wa tathmini mpya iliyowasilishwa leo. Taarifa kamili na Grace Kaneiya

Taarifa ya Grace Kaneiya

Kulingana na tathmini hiyo ya Ofisi ya Umoja wa Mataifa inayohusika na kupunguza hatari za majanga (UNISDR), nchi tano zilizoathiriwa zaidi na majanga mwaka 2015 ni Uchina, ambayo ilikumbwa na majanga 26, Marekani (22), India (19) Ufilipino (15) na Indonesia (11)

Mkuu wa ofisi hiyo, Robert Glasser, amesema watu milioni 98.6 waliathiriwa na majanga hayo yam waka 2015, na kwamba tabianchi na El Niño vilichangia asilimia 92 ya majanga hayo.

Amesema athari kubwa zaidi ilikuwa ni hali ya ukame ulioathiri watu milioni 50. Ukame ulishuhudiwa mara 32, ikiwa ni maradufu zaidi ya ukame uliorekodiwa kwa wastani wa miaka 10, na unaendelea hata mwaka huu, hususan barani Afrika.