Baraza la Usalama lalaani mashambulizi ya bomu yaliyofanywa na Boko Haram
Wajumbe wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, wamelaani vikali mno mashambulizi yaliyofanywa na Boko Haram mnamo Januari 30 2016 katika kijiji cha Dalori, kaskazini mashariki mwa Nigeria, ambayo yalisababisha idadi kubwa ya vifo na majeraha.
Taarifa ya Baraza la Usalama imesema wajumbe hao wameelezea rambirambi zao, na kuwapa pole familia na marafiki za waliouawa au kujeruhiwa katika mashambulizi hayo katili, pamoja na kwa watu na serikali ya Nigeria.
Aidha, wajumbe wa Baraza la Usalama wamepongeza juhudi za kikanda, zikiwemo kupitia kikosi kazi cha kimataifa, katika kupambana na Boko Haram, huku wakiunga mkono kuendelezwa kwa juhudi hizo.
Wamesema ugaidi wa aina yoyote ile ni moja ya tishio kubwa zaidi kwa amani na usalama wa kimataifa, wakikisisitiza haja ya kuwakabili kisheria waliotekeleza, pamoja na waliopanga au kufadhili vitendo hivyo.