Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hali iliyoko Mashiriki ya Kati si endelevu - Ban akariri

Hali iliyoko Mashiriki ya Kati si endelevu - Ban akariri

Msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Stéphane Dujarric amesema kwamba Katibu Mkuu Ban Ki-moon ameshikilia msimamo wake na kukariri kauli aliyoitoa kwenye Baraza la Usalama mnamo Jumanne Januari 26, kuhusu Mchakato wa amani Mashariki ya Kati.

Amesema hayo leo akizungumza na waandishi wa habari baada ya maoni kadhaa kuibuka kuhusu hotuba ya Katibu Mkuu, wengine wakimlaumu kwa kutetea ugaidi.

Bwana Dujarric ameeleza kwamba Katibu Mkuu anasisitiza kwamba hakuna kitu chochote kinachoweza kutetea ugaidi na kwamba jamii ya kimataifa inapaswa kushikamana ili kupambana na mizizi yake, huku akilaani mashambulizi dhidi ya raia wa Israel yanayofanywa na wapalestina.

Hata hivyo, Bwana Dujarric amekariri kauli ya Katibu Mkuu akimnukuu na kusema kwamba hali iliyoko hivi sasa si endelevu na hivyo:

(Sauti ya Bwana Dujarric)

“Tukitaka kuona mwisho wa ghasia, harakati za kiusalama hazitatosha. Tunapaswa kukabiliana na mizizi yake. Uchungu ulioenea na kushindwa kwa suluhu ya kisiasa. Baada ya miaka 50 ya kutawaliwa, Wapalestina, hasa vijana, wanakata tamaa.”