Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

India na Ufaransa kuunda setilaiti ya kuchambua tabianchi

India na Ufaransa kuunda setilaiti ya kuchambua tabianchi

India na Ufaransa zitaingia makubaliano ya kuunda setilaiti inayochambua mabadiliko ya tabianchi.

Hatua hiyo inafuatia mazungumzo kati ya Waziri Mkuu wa India Narendra Modi na Rais Francois Hollande wa Ufaransa ambapo taasisi mbili za masuala ya anga za juu za nchi hizo zitahusika na utengenezaji.

Mpango huu unaimarisha ushirikiano wa awali kati ya taasisi hizo za ISRO ya India na CNES ya Ufaransa ambapo tayari walishatengeneza setilaiti mbili za kutoa takwimu za uchambuzi wa tabianchi. Setilaiti hizo zinafuatilia vyanzo vya maji na uhakika wa chakula.

Kupitia tovuti ya ClimateAction inayofuatilia hatua za kudhibiti na kukabili mabadiliko ya tabia nchi, viongozi hao wawili walijadili wakati wa mazungumzo hayo nchini India jinsi ya kuhakikisha taasisi hizo mbili zinajikita zaidi kwenye hatua za kuhimili mabadiliko ya tabianchi.

Climate Action inaungwa mkono na shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira, UNEP.