Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kasi ya kuenea kwa kirusi cha Zika inatutia hofu- WHO

Kasi ya kuenea kwa kirusi cha Zika inatutia hofu- WHO

Mkurugenzi Mkuu wa shirika la afya duniani, WHO Dkt. Margaret Chan amesema taarifa za kuenea kwa kasi kwa kirusi cha Zika zinatia hofu kubwa .

Akizungumza kwenye kikao cha bodi ya wakurugenzi ya WHO, Dkt, Chan amesema hofu hiyo inazingatia uwezekano wa uhusiano unaodaiwa kuwepo kati ya kirusi hicho na watoto wanaozaliwa na vichwa vidogo.

Amesema ingawa hadi sasa hakuna uthitisho wa uhusiano kati ya kirusi hicho na watoto kuzaliwa na vichwa vidogo…

(Sauti ya Dkt, Chan)

“Ushahidi wa kimazingira unadokeza na unatia hofu sana. Ongezeko la kubainika kwa dalili za magonjwa ya mishipa ya fahamu katika baadhi ya nchi linaleta hali ya wasiwasi. Nashukuru mataifa yote yaliyopata kwa mara ya kwanza kirusi hicho na kutoa taarifa haraka na kwa uwazi kwa WHO kwa mujibu wa kanuni za afya za kimataifa.”

Mkuu huyo wa WHO amesema baadaye wiki hii msaidizi wake atawasilisha mbele ya bodi hiyo hatua ambazo shirika hilo imechukua hadi sasa kufuatia taarifa za Zika.

Kirusi hicho chenye asili ya msitu wa Zika huko Uganda kinaenezwa na mbu aina ya Aedes na kinapatikana pia Tanzania na huko Brazil ambako idadi ya walioambukizwa kirusi hicho inadaiwa kuongezeka kila uchao.