Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Matokeo ya uchaguzi wa wabunge yatangazwa CAR

Matokeo ya uchaguzi wa wabunge yatangazwa CAR

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati CAR, MINUSCA, umeripoti leo kuwa matokeo ya uchaguzi wa wabunge yametangazwa Jumanne hii na Tume ya Kitaifa ya Uchaguzi nchini humo.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini New York Marekani, msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Stéphane Dujarric amesema kwamba tayari wagombea 21 wakiwemo wanawake watatu wameshachaguliwa kwenye awamu ya kwanza ya uchaguzi baada ya kupata zaidi ya nusu ya kura.

Wakati huo huo Bwana Dujarric ameeleza kwamba MINUSCA inaendelea kuelimisha walinda amani kuhusu ukatili wa kingono, huku timu iliyoongozwa na Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu nchini humo Parfait Onanga-Anyanga ikiwa imetembelea vituo vinane vya polisi mjini Bangui ili kukariri msimamo mkali wa Umoja wa Mataifa kuhusu vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Halikadhalika, msemaji huyo wa Katibu Mkuu amesema kwamba shughuli za kusalimisha waasi zinaendelea kwenye majimbo kadhaa ya nchi.