Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mwakilishi wa haki za binadamu wa UM kufanya ziara ya mwisho Japan

Mwakilishi wa haki za binadamu wa UM kufanya ziara ya mwisho Japan

Mwakilishi maalumu wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu Jamuhuri ya watu wa Korea DPRK  Marzuki Darusman, atazuru Japan Januari 18 and 22 kutathimini maendeleo ya karibuni kuhusu DPRK na kujadili njia za kuhakikisha uwajibikaji wa ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu nchini humo ukiwemo vitendo vya utekaji.

Mtaalamu huyo huru ambaye muda wake utakwisha Julai mwaka huu aliteuliwa kwa mara ya kwanza na baraza la haki za binadamu mwaka 2010, hivyo hii itakuwa ziara yake ya mwisho Japan. Bwana  Darusman pia alikuwa mjumbe katika tume ya uchunguzi wa haki za binadamu kwa DPRK ambayo ilitoa ripoti yake mwezi Februari mwaka 2014.

Tangu alipoteuliwa mwakilishi huyo maalumu ametuma maombo mengi ya kuzuru DPRK lakini hadi sasa hakuna ruhusa aliyopewa. Amekuwa akizuru nchi nyingine katika ukanda kama Japan, Thailand na Jamhuri ya Korea.

Akiwa ziarani Japan atakutana na maafisa wa serikali, familia za watu waliotekwa, asasi za kijamii, waandishi wa habari na wadau wengine muhimu na atakuwa na mkutano na waandishi wa habari mwishoni mwa ziara yake.