Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kusini Mashariki mwa Asia wahitimisha miaka mitano bila Polio: WHO

Kusini Mashariki mwa Asia wahitimisha miaka mitano bila Polio: WHO

Shirika la afya ulimwenguni WHO limetangaza kuwa ukanda wa kusini mashariki mwa Asia umehitimisha miaka mitano bila kisa chochote cha polio na kusema ni hatua muhimu wakati huu ambapo ugonjwa huo unasalai tishio katika nchi nyingine.

Taarifa ya WHO inasema kuwa nchi katika ukanda huo zimepiga hatua kubwa za kishujaa katika kuwalinda watoto dhidi ya Polio na kwamba kisa cha mwisho kuripotiwa ilikuwa mwaka 2011 nchini India ambapo WHO ilitoa cheti cha kutokuwa na kisa chochote tarehe 27 Machi, 2014.

Shirika hilo la afya ulimwenguni limeonya kuwa hatua hiyo ni ukumbusho kuwa juhudi zaidi zinahitajika ili Polio itokomezwe kote duniani.

Ikiwa ni sehemu ya mkakati wakukomesha Polio nchi katika ukanda huo zinasongesha mbele chanjo dhidiya ugonjwa huo ili kuutokomeza ugonjwa hata katika visa vidogo vinavyoainishwa.