Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Dola Milioni 31 kusaidia wahitaji huko ziwa Chad

Dola Milioni 31 kusaidia wahitaji huko ziwa Chad

Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa inayohusika na usaidizi wa kibinadamu, OCHA Stephen O’Brien ameidhinisha dola Milioni 31 kwa ajili ya kusaidia mashirika ya kibinadamu yanayotoa misaada huko Nigeria na ukanda wa ziwa Chad.

Fedha hizo zinatoka mfuko wa dharura ya majanga wa Umoja wa Mataifa, CERF na unalenga kukabiliana na hali ya kibinadamu inayozidi kuzorota kwenye maeneo hayo kutokana na ghasia zinazochochewa na kikundi cha kigaidi cha Boko Haram.

Umoja wa Mataifa umesema watu wengi wenye uhitaji wamepoteza kila kitu, maelfu ya wanawake na watoto wanaendelea kubeba mzigo wa athari za mzozo huo na hapa msemaji wa OCHA Jens Learke anafafanua lengo la msaada huo.

(Sauti ya Jens Laerke)

Kuimarisha mipango yao ya kusaidia wahanga waliopoteza makazi na kuathiriwa na janga hili na wanahitaji msaada haraka. Tunafahamu watu wanahitaji chakula, maji safi, afya na elimu, lakini muhimu kabisa wanahitaji ulinzi kutokana na kile kinachoendelea.”

Tangu kuanzishwa kwake mwaka 2006, CERF imeshatoa dola bilioni 4.2 kusaidia operesheni za misaada ya kibinadamu kwenye mataifa 94.