Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Idadi ya waliozama Mediteranea wiki moja ya mwaka huu yatisha:IOM

Idadi ya waliozama Mediteranea wiki moja ya mwaka huu yatisha:IOM

Shirika la kimataifa la uhamiaji, IOM limesema wiki moja tangu kuanza kwa mwaka mpya wa 2016, idadi ya wahamiaji au wakimbizi waliofariki dunia au kupotea kwenye bahari ya Mediteranea imefikia 46, wengi wao wakikumbwa na zahma hiyo kwenye meli pwani ya Uturuki siku ya Jumanne.

Akizungumza mjini Geneva, Uswisi na waandishi wa habari msemaji wa IOPM Joel Millman amesema haifahamiki wahamiaji hao walikuwa kwenye vyombo gani vya usafiri, halikadhalika idadi yao.

(Sauti ya Joel)

“Tuko wiki moja tu ndani ya mwaka mpya, na tayari tumerekodi watu 46 kuzama katika bahari ya mediterenia, hiyo siyo takwimu kubwa kwa mwaka lakini kwa wiki moja ni kubwa sana, ni zaidi ya matukio ya mwezi mzima wa januari mwaka jana, na ni sawa na takwimu ya miezi mitatu ya mwaka 2014, kwa hiyo ni tukio la kutia wasiwasi mkubwa.”